Habari kutoka Libya zinasema kuwa dikteta wa Libya Kanali Muammar Gaddafi amefariki dunia baada ya kujeruhiwa vibaya kichwani na miguuni alipokuwa akijaribu kutoroka kutoka mji wa Sirte. Habari zaidi zinasema kuwa Gaddafi akiwa kwenye msafara mkubwa wa magari alijaribu kutoroka punde baada ya wanamapinduzi wa Libya kuutwaa kikamilifu mji wa Sirte mapema leo. Baadaye ndege za kivita za NATO ziliufuata msafara huo na kuudondoshea mabomu ambapo Gaddafi alijeruhiwa vibaya kichwani na miguuni. Imeripotiwa kuwa wapiganaji wanamapinduzi walimkamata Gaddafi akiwa hai lakini akafariki baadaye kutokana na majeraha. Video inayowaonyesha wanamapinduzi wakiuburuza mwili wa Gaddafi imeenea katika kanali za televisheni na kwenye intaneti. Kamanda wa ngazi za juu wa jeshi la wanamapinduzi Abdel Majid Mlegta amethibitisha kufariki dunia kanali Gaddafi na kusema kuwa ushahidi wa picha na video umetolewa hadharani. Msemaji wa Baraza la Mpito la Libya Abdel Hafez Ghoga pia amethibitisha kuuawa Gaddafi.